Zaidi ya kaya 100 zimepoteza makazi katika Wilaya ya Sumbawanga Vijijini, mkoani Rukwa, baada ya mvua kubwa iliyoambatana na upepo mkali kuharibu nyumba na mali za wananchi.
Wakazi wa Kata ya Mtowisa wamesema mvua hiyo iliyonyesha jana Machi 17, 2026, ilianza saa mbili usiku na kusababisha baadhi ya nyumba kuezuliwa mapaa huku nyingine zikianguka. Pia, mashamba takribani ekari 600 yameharibiwa.
Wananchi wameishukuru Serikali ya Wilaya kwa jitihada za kuwasaidia, huku Ofisa Tarafa ya Mtowisa, Aida Mzee akisema waathirika wamehifadhiwa kwa ndugu zao wakisubiri utaratibu zaidi wa msaada.
Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga, Nyakia Ally Chirukile amewataka wananchi kuzingatia kanuni za ujenzi na kutunza mazingira ili kupunguza madhara ya majanga.
Amesisitiza upandaji miti na kuepuka ujenzi mabondeni. Aidha, Kamati ya Maafa ya Wilaya imeagizwa kufanya tathmini ya kina ili kubaini hasara na kupanga namna ya kusaidia waathirika.
Chanzo; Mwananchi