dunia inaadhimisha Siku ya UKIMWI Duniani tangu kuanzishwa kwake mwaka 1988, ikiwa ni miaka 37 sasa ya kampeni za kupambana na janga hili linaloendelea kuathiri mamilioni ya watu.
Kaulimbiu mbalimbali zimekuja na kupita, lakini lengo limebaki lile lile: kuzuia maambukizi mapya, kulinda waliokuwa katika hatari na kuwezesha jamii kuishi na watu wenye Virusi vya UKIMWI (VVU) bila unyanyapaa.
Katika kuadhimisha siku hii muhimu, simulizi ya Mzee Douglas Kisunga (72), mkazi wa Isanga jijini Mbeya, inaibuka kama moja ya hadithi za kipekee zinazovunja hofu na kuonesha kwamba kuishi na VVU si hukumu ya maisha kukoma. Ni hadithi ya maisha ya zaidi ya miaka 32 ya ujasiri, uamuzi mgumu na mapambano ya kibinadamu.
HOFU ILIPOANZA
Tanzania ilipogusia kwa mara ya kwanza kuwapo maambukizi ya VVU mapema miaka ya 1980, hofu ilikuwa juu kuliko uelewa. Rais wa wakati huo, Hayati Ali Hassan Mwinyi, alitangaza kuwa ni janga la kitaifa na kwa kweli, jamii ilikumbwa na mshtuko.
Watu waliokutwa na virusi hivyo walijikuta wakikumbwa na unyanyapaa, wengine wakikataliwa na familia zao na wengi wakiona kwamba mwisho wa maisha yao umefika. Katika hali hiyo ya sintofahamu ndipo safari ya Mzee Kisunga ilipoanza.
Kabla ya mwaka 1993, Mzee Kisunga alikuwa mwalimu wa shule za msingi katika Wilaya ya Mbeya, akiwa ameijenga taaluma yake kwa miaka mingi. Lakini ghafla, mapema mwaka huo, afya ilianza kudorora bila sababu inayoeleweka.
"Nilikuwa ninaumwa, lakini madaktari hawakuweza kuelewa chanzo. Wakanishauri nipime VVU… ilikuwa ni hofu tupu," anasema.
Ilipofika siku ya kupokea majibu, zile dakika chache za kusubiri mtihani mgumu. Hatimaye, alielezwa kuwa ana maambukizi. Ndani yake kulijaa wingu jeusi.
"Nilinyong’onyea. Nilijiona kama nimeshafariki dunia. Niliogopa hata kivuli changu," anasimulia.
Chanzo; Nipashe