Tanzania iko mbioni kuanza ujenzi wa minara mipya 600 katika maeneo ya vijijini na pembezoni ambayo hayajafikiwa kikamilifu na huduma ya mtandao na intaneti.
Mradi huu wa awamu ya pili ni baada ya kukamilika kwa awamu ya kwanza ya ujenzi wa minara 758 iliyowanufaisha wananchi milioni 8.5 katika mikoa 26, wilaya 128, kata 688 na vijiji 1,404.
Hayo yamewekwa wazi leo Jumatano, Machi 18, 2026 katika ziara ya Kamati ya kudumu ya Bunge Miundombinu katika moja ya minara iliyojengwa eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam.
Kufuatia mradi huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Selemani Kakoso amesema wakati awamu ya pili ya ujenzi wa miundombinu hii ikiwa katika mchakato wa kuanza ujenzi ni muhimu kusimamia viwango vya ujenzi wa minara hiyo ili kuhakikisha inaleta tija iliyokusudiwa kwa wananchi.
“Ubora wa huduma uzingatiwe, minara iliyojengwa asilimia kubwa haina ubora unaokusudiwa kwani baadhi ya maeneo mpakani kunakuwa na minara ya kampuni za Tanzania lakini watu wanapata mawasiliano ya nje kuliko mnara uliopo,” amesema.
Chanzo; Mwananchi