Jeshi la Polisi mkoani Shinyanga linamshikilia Mkazi wa Mtaa wa Mageuzi Manispaa ya Shinyanga, Mwajuma Shaban (24), kwa tuhuma za kumchoma moto mumewe, David Mollis (34) kwa madai ya wivu wa mapenzi.
Akizungumza tukio hilo juzi, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Janeth Magomi, alisema tukio hilo lilitokea Machi 5 mwaka huu majira ya saa sita usiku.
Kamanda Magomi alisema chanzo cha tukio hilo ni wivu wa mapenzi, ambapo mwanamke huyo, alidai alimkopesha mumewe Sh.80,000 na kuhisi hela hizo (mumewe) amempelekea mwanamke mwingine, ndipo alipochukua maamuzi ya kumchoma moto.
“Wakati mwanaume huyo akiwa amekaa sebuleni na kujipumzisha, mke wake alimmwagia mafuta ya petroli, kisha kumchoma moto, ndipo akakurupuka usingizini na kuanza kuomba msaada,” alisema Kamanda Magomi.
Alisema baada ya kuchomwa moto alipata majeraha sehemu mbalimbali za mwili wake ikiwamo kifuani, na alikimbizwa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Alisema, Jeshi la Polisi linamshikilia mwanamke huyo kwa mahojiano zaidi na uchunguzi utakapokamilika atafikishwa mahakamani kwa hatua zaidi za kisheria.
Alisema Jeshi la Polisi linalaani vitendo vya ukatili na kutoa wito kwa wanandoa pamoja na jamii kuepuka migogoro inayoweza kusababisha madhara makubwa, badala yake kutumia njia za kisheria kutatua matatizo.
“Jeshi la Polisi tuna dawati la jinsia la kushughulikia masuala ya ukatili, tunawaomba wananchi wenye migogoro ya ukatili wafike polisi ili kutatufa suluhu,” alisema Kamanda Magomi.
Chanzo; Nipashe