Rais wa Marekani Donald Trump amewakosoa viongozi wa Ulaya kwa kuwaita dhaifu na kusema Marekani inaweza kupunguza msaada kwa Ukraine.
Katika mahojiano ya kina na mtandao wa habari Politico, Trump amesema nchi za Ulaya dhaifu zimeshindwa kudhibiti uhamiaji au kuchukua hatua madhubuti kukomesha vita vya Ukraine na Urusi, akiwashutumu kwa kuiacha Kyiv ipigane hadi ianguke.
Aidha, anaelezwa kuwa viongozi wa Ulaya wamefanya majaribio ya kuonyesha jukumu katika juhudi zinazoongozwa na Marekani za kukomesha vita hivyo, ambavyo wanahofia vitaathiri maslahi ya muda mrefu ya bara hilo kwa ajili ya suluhisho la haraka.
Akijibu hoja hiyo, Waziri wa Mambo ya kigeni wa Uingereza Yvette Cooper amesema alichokiona barani Ulaya ni uimara, akitoa mfano wa uwekezaji katika ulinzi pamoja na ufadhili kwa Kyiv.
Aliongeza kuwa marais wawili walikuwa wakishughulikia mchakato wa amani akimrejelea Trump na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky huku Rais wa Urusi Putin hadi sasa akiendelea kuzidisha mgogoro huo kwa kutekeleza mashambulizi zaidi ya ndege zisizo na rubani na makombora.
Chanzo; Nipashe